Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa Azam FC umeweka wazi siri yao ya kucheza michezo nchini Rwanda ni kocha wao,Florent Ibenge kuangalia uwezo wa kila mchezaji ndani ya kikosi chake.
Ofisa Habari na Mawasiliano wa Azam, Hashim Ibwe alisema hayo alipozungumza na baadhi ya vyombo vya habari kuwa kocha wao, amekuwa anatumia michezo hiyo kuangalia kiwango cha wachezaji kabla ya kuanza msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2025/26.
“Unajua kocha wetu ana uwezo mkubwa, tayari amefahamu udhaifu wa kikosi chetu na anaendelea kufanyia kazi katika mazoezi.
“Mechi tulizocheza zilikuwa na umuhimu mkubwa katika timu na kocha ameona mapungufu ya wachezaji anafanyia kazi ya kuboresha,” alisema.
Ofisa huyo aliongeza kwamba msimu mpya wa ligi utakuwa na ushindani mkubwa kutokana na kusajili wachezaji wazuri.
“Msimu mpya wa ligi utakuwa na ushindani mkubwa hivyo watu wategemee mambo mazuri kutoka Azam maana vitu vizuri vinakuja kutoka kwetu,” alisema.



